TANGAZO ISERESPORTS COLLECTION

TANGAZO SHIWATA

Sunday 1 March 2015

Kikwete aomboleza kifo cha Komba



Na Peter Mwenda

RAIS Jakaya Kikwete na mkewe Salma Kikwete jana waliongoza  waombolezaji waliofika kuhani na kusaini kitabu cha maombolezo nyumbani kwa marehemu Mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi, Kepteni John Komba aliyefariki juzi kwenye Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam.

Marehemu Komba ambaye alifariki kwa shindikizo la Damu (BP) na Kisukari anatarajiwa kuagwa leo katika viwanja vya Karimjee kuanzia saa 4 asubuhi na baadaye safari ya kwenda nyumbani kwao Mbinga kwa mazishi yanayotarajiwa kufanyika Kesho kutwa.

Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Lowassa katika salamu za rambirambi alimtaja marehemu Komba kuwa alikuwa mtu muhimu kwa Chama cha Mapinduzi (CCM) na watanzania wote kwa sababu alitumia kipaji chake cha kuimba kuwaunganisha na kuwaburudisha.

Lowassa alisema kwa upande wake, marehemu Kepteni Komba alikuwa mtu muhimu kwani alifanya kazi za CCM kwa nguvu na moyo wake na kukifanya chama hicho kipoteze muhamasishaji katika mambo mbalimbali ya jamii.

Naye Katibu Mkuu wa CHADEMA, Willibroad Slaa alisema kifo cha Kepteni Komba ni cha watanzania wote bila kujali chama kwa sababu marehemu alikuwa msanii mwenye kipaji cha hali ya juu kuburudisha watanzania.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam,Ramadhani  Madabida alisema CCM imepata pigo kubwa lakini kwa sababu kila mwanadamu aliandikiwa siku ya kuzaliwa na kufa kwake hakuna budi kukubali matakwa ya Mungu kuwa amemchukua anayempenda.
Marehemu Komba ambaye alikuwa asafiri jana kwenda nchini Ethiopia katika Kamati ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto akiwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo imelezwa kuwa kifo chake kimetokea ghafla.
Wengine waliofika kuhani msiba wa Komba ni Spika wa Bunge, Anna Makinda ambaye alisema marehemu alikuwa mchapa kazi na mwadilifu na hakuwa mtu wa majungu katika vikao vya bunge na Waziri wa Mambo ya Ndani, Hussein Mwinyi alisema marehemu alikuwa akijitahidi kuhakikisha wananchi wa Jimbo lake wanapata huduma muhimu.
Naibu Waziri wa Fedha, Mwingulu Mchemba, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Hawa Ghasia, wabunge wa Chadema jimbo la Arumeru, Joshua Nasari, Mbunge wa Arusha mjini, Godles Lema na waombolezaji wengine.
Msemaji wa Kampuni ya TOT Plus, Gasper Tumaini alisema mwili wa marehemu Komba ulitarajiwa kuwasili nyumbani kwake jana saa 11 jioni kwa ajili ya kuagwa na waombolezaji ambao hawatapata nafasi  kesho na baadhi ya ndugu, jamaa na marafiki walitarajiwa kuondoka jana jioni.

Tumaini alisema kutakuwa na mabasi sita yatakayochukua waombolezaji na magari mengine matatu ambayo yatatangulia na mwili utafuata kesho kwa ndege baada ya heshima za mwisho Karimjee.

mwisho





No comments:

Post a Comment