SHIWATA yaipongeza Serikali kutambua kijiji chao Mkuranga
Na Mwandishi Wetu, Mkuranga
SERIKALI imepongezwa kwa kutambua juhudi
zinazofanywa na wasanii, wanamichezo na waandishi wa habari za kujenga
nyumba za makazi katika kijiji cha Mwanzega Mkuranga ambapo Mwenge wa
Uhuru ulifika na kuweka jiwe la msingi Julai 22 mwaka huu.
Mwenyekiti wa Mtandao wa Wasanii Tanzania (SHIWATA),Cassim Taalib
katika risala aliyosoma mbele ya Kiongozi wa Mwenge kitaifa, Rachael
Kassanda alisema Serikali kukitambua kijiji hicho kumeongeza ari ya
wasanii kujenga nyumba za kisasa na kuongeza kasi ya maendeleo.
Alisema kijiji cha wasanii kimeanzishwa mahususi kwa ajili ya
kuwakomboa na kuwapatia makazi ya kudumu wakisha staafu au kupotea kwa
umaarufu wao katika fani zao.
Katika sherehe hizo ambazo wasanii
zaidi ya 1,500 waliofurika kupokea mwenge wa uhuru kiongozi wa mbio za
Mwenge, Rachael Kassanda aliwatoa wito kwa wasanii kuwa kioo halisi cha
jamii kwa kuiga mema na kupiga vita mabaya katika jamii zinazowazunguka.
Awali Mkuu wa wilaya ya Mkuranga, Mercy Sila aliwaasa wasanii
kutumia vipaji vyao kuwaelimisha jamii kuhusu maadili mema na kuiga
yanayostahili kwa mila na desturi za Mtanzania.
Katika sherehe za
kuweka jiwe la msingi zilizofanywa na kiongozi wa mbio za
Mwenge,SHIWATA ilimsimika balozi wa kijiji hicho kuwa ni msanii maarufu
na mtangazaji wa kituo cha Redio Times FM, Suzan Natasha ambaye aliahidi
kukitangaza kijiji hicho katika mipaka ya ndani na nje ya Tanzania.
Sherehe hizo zilizoambatana na burudani mbalimbali zilizongozwa na
Bendi ya Polisi, wanamuziki maarufu Kikumbi Mwanzo "King Kikii", Siza
Mazongera "Wana Segere" na wasanii mbalimbali walitumbuiza.
Wengine walioshudia kuwekwa jiwe la msingi katika kijiji hicho
baadhi yao ni wachezaji wa zamani wa Simba, Moses Mkandawile, George
Lucas,Thom Kipese na kwa upande wa Yanga ni Abeid Mziba, Ramadhani
Kampira, Bakari Malima, Omari Husein na wengineo.
Pia katika kusherekea mwenge wa uhuru SHIWATA ilitoa ofa bure kwa
wanachama wapya kupimiwa viwanja vya kujenga nyumba bure katika kijiji
hicho ambapo wanamichezo, wasanii na waandishi wa habari walipata fursa
ya kuoneshwa viwanja watakavyotakiwa kujenga.
mwisho
No comments:
Post a Comment